Makala

Historia ya Valentine Day pamoja na umuhimu wake

0
Historia Valentine Day
Siku ya Wapendanao

Valentine Day ni siku inayoadhimishwa kila mwaka ifi kapo Februari 14. Imetokana na Mtakatifu, Askofu wa Kanisa Katoliki wa miaka ya 496 Baada ya Kristo aliyeitwa Valentine.

Siku hii watu wengi huiadhimisha kwa kupeana zawadi mbalimbali kama kadi, maua na nyingine nyingi zenye ishara ya upendo.

Katika kipindi hicho Papa Gelasius alidhamiria kumuenzi Valentine kwa kuweka Februari 14 kuwa Siku ya Wapendanao duniani kuanzia Karne ya 14. Maandishi hayo yanaishi mpaka leo.

Hata hivyo, licha ya watu wengi kuadhimisha siku hii kwa mbwembwe, bado wengi hawajui historia, maana na lengo hasa la Siku ya Wapendanao.

Kimsingi, hii ni siku ya kumkumbuka Padri Valentine aliyeuawa na Utawala wa Kirumi sababu ya kutetea waumini waweze kufunga ndoa.

ILIKUWAJE?

Katika miaka hiyo kulikuwa na vita kama ilivyokuwa desturi ya falme nyingine ili ziweze kujipanua.

Mfalme Cladius ll naye alikuwa mtawala aliyependa sana kupigana vita na majirani zake katika kile kinachoitwa kukuza eneo analolitawala. Inaelezwa katika vyanzo mbalimbali kuwa, katika utafiti mdogo alioufanya Cladius, aligundua kuwa wanajeshi wasiooa, ndio walikuwa imara kuliko waliooa.

Ikambidi mtawala huyu azuie ndoa kwa kipindi kile ili kupata wapiganaji watakaomfanya ashinde vita dhidi ya maadui zake kwani pia aliamini kuwa, askari waliooa pia wasingeweza kuwa huru kufanya majukumu ya familia na vita.

Ndipo Cladius akaweka marufuku na kuwataka vijana wasifunge ndoa badala yake, wajiunge katika jeshi.

Soma pia:  Kamari inavyoliza maelfu na kumchekesha mmoja

Mmoja ameandika katika mtandao akisema: “Kwa mtazamo wa Valentine, yeye aliona kuwa kukataza ndoa ni kuongeza uzinzi ndani ya Roma, hivyo akakataa kutii amri na badala yake, akaendelea kufungisha watu ndoa kwa siri.”

Baada ya muda kupita, Mfalme Cladius akapata taarifa mintarafu mambo ya siri anayoyafanya Padri Valentine kwa kufungisha ndoa.

Akaagizwa akamatwe na kumtaka Valentine aachane na kile anachokifanya na asiabudu katika Yesu. Valentine akabaki katika msimamo wake wa kumwamini Yesu.

Habari zinasema baada ya msimamo huo, Mfalme akamhukumu Valentine adhabu ya kifo. Wakati akiwa jela akisubiri siku yake ya kunyongwa Valentine alikuwa akitembelewa na vijana waliokuwa wakimpelekea maua kuonesha wako pamoja nae.

Inasemekana akiwa gerezani alimpenda binti kipofu aliyekuwa mtoto wa msimamizi wa gereza alipokuwa amefungwa.

Mara kadhaa binti huyo kipofu alikuwa akihudhuria gerezani ili kumuona Padri Valentine. Kwa muda kadhaa, Valentine alikuwa akimtumia binti salamu akiwa gerezani na ndiyo dhana ya sikukuu hii.

Mmoja wa vijana waliokuwa wakienda kumtembelea ni mtoto wa mkuu wa gereza ambaye aliruhusiwa kuingia mpaka kwenye selo la Valentine “kupiga naye stori”.

Inasemekana kwamba Valentine aliangukia katika mapenzi na binti huyo wa mkuu wa gereza wakati anasubiri kunyongwa.

Inasemekana kwamba muda mchache kabla hajanyongwa, Valentine aliomba kalamu na karatasi na kuandika ujumbe wa kumuaga aliyoihitimisha kwa maneno: “From Your Valentine” (kutoka kwa Valentine wako) kama maneno haya yanavyotumika sana katika siku hii. Valentine akanyongwa tarehe 14 Februari mwaka 269 AD.

Soma pia:  Baking soda tiba ya Kusafishia sehemu chafu bafuni

Baada ya kunyongwa kwa Valentine, vijana wa Roma walianza kumuiga Valentine na kuwaandikia na kuwatumia wanawake waliowapenda salamu za mapenzi.

Tangu siku hiyo tarehe hiyo ikaanza kuhusishwa urafiki, upendo na mahaba duniani huku ikihusishwa zaidi na mambo ya mapenzi.

Siku hiyo imezidi kuwa maarufu kila miaka inavyoenda huku makampuni yakiigeuza siku hiyo kuwa ya biashara zaidi kwa kufanya kila kitu maalumu kwa Siku ya Wapendanao kionekane kuwa inabidi kiwe chekundu kuanzia kadi za salamu, maua, mpaka nguo wavaazo.

Valentine alionesha upendo, heshima, hekima na unyenyekevu kwa kile alichokiamini yaani Ukristo. Alionesha msingi imara katika utetezi wa mapenzi katika ndoa kwani ni kitu muhimu duniani kiasi kwamba, ikambidi kukataa kumtii mfalme kwa ajili ya kutetea ndoa.

Wakristo wakaweka siku ya kumkumbuka Padri Valentine kama mfiadini kwa kutetea maisha ya Wanakanisa kuwa wanandoa. Siku hii ikaenea katika Kanisa nchi za Magharibi na hata duniani ambako Wanakanisa wanamkumbuka Mtakatifu Padre Valentine.

Baadaye ikapokewa na watu hata wasio na imani ya Kikristo kama ni siku ya kufanya kumbukumbu kwa Valentine kama mtetezi wa ndoa. Ndipo baada ya miaka kadhaa kupita, Kanisa Katoliki likamtangaza kuwa mtakatifu na ndiyo maana anaitwa Mtakatifu Valentine.

CHANZO CHA UPOTOFU KUHUSU SIKU YA WAPENDANAO

Inaelezwa kuwa, miaka michache baadae, Sikukuu ya Wapendanao ilibeba maudhui au uzito wa mapenzi zaidi kuliko maana halisi.

Soma pia:  Mradi wa Pasipoti ya Kielektroniki pamoja Faida zake

Kati ya Karne ya Tano na Karne ya 15, katika nchi za Uingereza na Ufaransa iliaminika kuwa, Februari 14 ndiyo iliyokuwa mwanzo wa kipindi cha ndege kutaga mayai.

Imani hii ikajenga dhana miongoni mwa watu kwamba, Siku ya Valentine lazima iwe siku ya kuonesha mapenzi baina ya wanawake na wanaume kingono na hii, ndiyo sababu ndege hutumika pia kama alama ya Valentine.

MUHIMU KUZINGATIA

Watu na machapisho mbalimbali yanaielezea Siku ya Wapendanao kuwa siyo siku ya watu kustarehe kingono na kufanya ufuska unaowahitimisha katika umaskini, magonjwa ya zinaa, Ukimwi na hata migogoro ya kisheria, bali kuimarisha na kujenga upendo wa agape kwa watu mbalimbali.

Hawa, wanaweza kuwa wazazi, ndugu, majirani na wafanyakazi au wanafunzi wenzako.

Kimsingi, hii ni siku nyingine ya kuanza kutenda mema zaidi kwa watu hasa wenye shida na wahitaji mbalimbali.

Unaweza kuonesha upendo kwa kutembelea wagonjwa, wafungwa, yatima na wengine wenye mahitaji maalumu na waliovunjika mioyo.

Tumia ulicho nacho kushiriki nao, badala ya kukitumia kwa uzinzi na uasherati ambao mara zote, huhitimishwa kwa majuto hata ya kimya kimya na hivi, vyaweza kuwa vyakula au mavazi hata yale unayoamini kwamba, hutaweza kuyatumia kama nguo na viatu.

Kila mmoja azingatie kuwa, siku hii imelenga kuhamasisha watu kupendana. Hii ni kusema kuwa, unaweza kuonesha upendo kwa mtu yeyote, si lazima awe mwenza wako.

Comments

Comments are closed.

More in Makala