Michezo

Bondia afariki dunia baada ya kichapo

0
Bondia afariki dunia kichapo
Maxim Dadashev

Bondia raia wa Urusi, Maxim Dadashev, amefariki dunia baada ya pambano lake na Subriel Matias kumsababishia majeraha makubwa ya ubongo.

Dadashev mwenye miaka 28, alishindwa kutembea mwenyewe baada ya pambano hilo ambalo kocha wake, Buddy McGirt alilazimisha lisimamishwe katika raundi ya 11 baada ya bondia huyo kupokea kichapo kikali bila majibu.

Pambano hilo lilipigwa Ijumaa wiki iliyopita na punde tu baada ya pambano hilo, Dadashev alikimbizwa hospitali.

Madaktari waligundua kuwa damu ilikuwa ikimvuja kwenye ubongo na kufanyiwa upasuaji wa haraka, lakini akafikwa na umauti juzi Jumanne.

Shirikisho la ndondi la Urusi limesema tayari uchunguzi umeshafuguliwa juu ya mkasa huo. Katibu Mkuu wa shirikisho hilo, Umar Kremlev amedai kuwa kulikuwa na aina fulani ya uvunjwaji wa taratibu.

Soma pia:  Mwanafunzi Kutoka Tanzania Auwawa Afrika Kusini

“Tutaiunga mkono familia yake, ikiwemo kifedha. Tutakamilisha uchunguzi wa kuangalia mazingira ya pambano, tunahitaji kujua ukweli wa kilichotokea. “Hili linaweza kutokea kwenye mchezo wowote. Naamini kuna mapungufu ya kibinadamu yamechangia kuwapo na aina fulani ya uvunjwaji wa taratibu,” alisema Umar.

Dadashev ambaye alikuwa akifanya shughuli zake za masumbwi nchini Marekani alishinda mapambano yake yote 13 aliyoyacheza kabla.

Ijumaa alipambana na Matias kutoka Puerto Rico katika jimbo la Maryland ambapo alisukumiwa makonde mazito na kwa kasi kali.

Kocha McGirt alieleza kuwa baada ya pambano alishindwa kumshawishi kukubali kushindwa, lakini akaamua kurusha taulo ulingoni baada ya kuona akipigwa zaidi za zaidi kwa makonde ya wazi kadri pambano lilivyokuwa likiendelea.

Comments

Comments are closed.

More in Michezo